Bulaya Amtaka Wasira Mahakamani




By Jesse Mikofu, Mwananchi
Mwanza. Mbunge wa Bunda Mjini (Chadema), Ester Bulaya amemtaka aliyekuwa mpinzani wake katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana, Stephen Wasira (CCM) kuacha kujificha nyuma ya wapigakura, badala yake ajitokeze kortini kupinga ushindi wake.
Kupitia kwa wakili wake, Tundu Lissu, mbunge huyo alidai mbele ya Jaji Ramadhan Mohamed wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza kuwa, ingawa jina la Wasira halimo kwenye orodha ya wadai, lakini ametajwa kwenye hoja zote za walalamikaji ambao pia wamekiri kwa hati ya kiapo kuwa hoja walizowasilisha mahakamani walizipata kutoka kwake.
Bulaya alikuwa akiwasilisha hoja za pingamizi aliloweka dhidi ya shauri la madai namba moja la mwaka 2015 lililofunguliwa mahakamani hapo na Magambo Masato na wenzake watatu wakiiomba mahakama kutengua matokeo yaliyompa ushindi mbunge huyo aliyekuwa kada wa CCM kabla ya kuhamia Chadema.
“Kwa nini Wasira asijitokeze mwenyewe kuja mahakamani kudai haki yake iliyokiukwa badala ya kujificha nyuma ya wapigakura ambao kimsingi walipata haki yao ya kikatiba ya kupiga kura?” alihoji Lissu.
Wakili huyo alidai maelezo yote kwenye hati ya madai ya walalamikaji hayataji haki yoyote ya mpigakura iliyokiukwa, bali anayedaiwa kunyimwa haki ni Wasira ambaye siyo mmoja wa walalamikaji.
Bulaya anaiomba mahakama hiyo kutupilia mbali maombi hayo akidai walalamikaji hawana haki kisheria kupinga matokeo ya uchaguzi.
Miongoni mwa madai ya msingi ya walalamikaji wanaowakilishwa na mawakili Constantine Mutalemwa na Denis Kahangwa, wanadai Wasira alikataliwa ombi la kuhesabu wala kuhakiki kura.
Walalamikiwa wengine ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Bunda Mjini. Uamuzi wa pingamizi hilo utatolewa Januari 25.

SOURCE: GAZETI LA MWANANCHI
PICHA: MWANANCHI 


EmoticonEmoticon