MAALIM SEIF: ZANZIBAR,BAR ZIPOKEZANE URAIS


Dar es Salaam. Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema kwa mfumo wa muungano uliopo, ni vyema kila upande ukawa unatoa rais kila baada ya miaka 10.
Amesema haiwezekani ziwepo nchi mbili zilizoungana halafu kila akichaguliwa rais awe anatokea upande mmoja tu wa muungano, huku upande mwingine ukiambulia kutoa makamu wa rais.
Mbali na hilo, Maalim Seif pia ametaja sifa tano za rais ajaye huku akisisitiza kuwa kigezo si umri, bali uwezo wake wa kufanya kazi.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili Dar es Salaam, Maalim Seif alisema: “Kama ni muungano wa nchi mbili lazima kuwe na mfumo ambao tutajua kwamba kipindi hiki rais ametokea Zanzibar, basi kipindi kingine rais atatoka Bara.”
Tangu Tanganyika na Zanzibar zilipoungana na kuzaliwa Tanzania mwaka 1964, Rais wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi ndiye pekee ambaye alitokea Zanzibar. Aliongoza kati ya mwaka 1985-1995.
Akizungumzia Serikali ya Umoja wa Kitaifa kama inaweza kutumika Tanzania Bara, kwa umakini Maalim Seif alisema, “Hilo ndilo suluhisho kutokana na mivutano iliyopo Tanzania Bara. Serikali hii inaunganisha vipaji vya watu ambao wanafanya kazi kwa pamoja.”
Sifa za rais
Huku akiwa makini na kuonyesha msisitizo wa ishara za mikono, Maalim Seif alisema: “Kwanza rais awe na uwezo wa kuunganisha wananchi kwa sababu ni wa Watanzania wote, kuanzia waliompigia kura na ambao hawakumpigia kura. Asiwe na upendeleo.”
Alisema mtu akishakuwa rais lazima aweke masilahi ya chama chake pembeni na awatumikie wananchi wote.
“Pili, rais anatakiwa kuwa karibu na wananchi kwa sababu sifa za kiongozi mzuri ni kujua hali halisi ya wale unaowaongoza, huwezi kujua hali halisi maisha ya wananchi kama hauko karibu nao,” alisema.
Akitaja sifa ya tatu huku akicheka, Maalim Seif alisema rais ni lazima awe na uamuzi na kuhakikisha kuwa anawabana watu aliowateua.
“Simaanishi rais awe dikteta. Rais unaweza kuwa na baraza lako la mawaziri lakini lazima uwe na malengo yako. Mawaziri wako unawaeleza wazi kwamba katika sekta fulani unataka jambo fulani lifanikiwe, jambo hilo linapendekezwa na kujadiliwa katika kikao cha mawaziri na hatimaye kupitishwa.”
source:Mwananchi


EmoticonEmoticon