RASIMU YA WARIOBA YACHANWACHANWA

Dodoma. Kuna kila dalili kwamba mabadiliko mengi yaliyopendekezwa katika Rasimu ya Katiba yakigusa miundo ya taasisi nyeti za umma yatawekwa kando na huenda Bunge Maalumu likatoa Katiba isiyokuwa na mabadiliko makubwa kama ilivyotarajiwa.
Gazeti hili limebaini kuwa kamati nyingi za Bunge hilo zimebadili mapendekezo mengi hasa yanayowagusa viongozi na taasisi nyeti kama Bunge, tofauti na ilivyopendekezwa katika Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya uongozi wa Jaji Joseph Warioba.
Miongoni mwa mambo ambayo yamependekezwa kurejeshwa kama yalivyokuwa ni muundo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambalo kwa mujibu taarifa kutoka kwenye kamati mbalimbali, ni kuendelea na muundo wa sasa unaowajumuisha wabunge kutoka Zanzibar.
Katika maelezo yake, Jaji Warioba alisema moja ya kero za muungano katika eneo la Bunge ni malalamiko kwamba wabunge kutoka Zanzibar wamekuwa wakishiriki katika Bunge la Muungano na kushiriki kujadili mambo yanayohusu Tanzania Bara.
Kupitia mfumo wa Serikali tatu, Rasimu ilikuwa na mapendekezo ya kuwapo kwa Bunge la Muungano lenye wabunge 75, lakini mapendekezo hayo pia yamefutwa katika kamati karibu zote na kurejesha mfumo wa sasa pamoja na uwapo wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.
Mwenyekiti wa Kamati Namba Tano, Hamad Rashid Mohamed alisema jana kuwa suala la muundo wa Bunge lilisababisha mvutano mkubwa katika kamati yake na baadhi ya wajumbe walikuwa wakihoji uwakilishi mkubwa wa wabunge wa Zanzibar katika Bunge la Muungano hata kwa mambo ya Tanzania Bara.
Hata hivyo, alitetea hali hiyo akisema uwapo wa wabunge kutoka Zanzibar ni moja ya masharti yaliyowekwa na Katiba. “Hata Katiba ya sasa imeweka sharti la idadi ya wabunge wa Zanzibar, hilo nalo ni sharti la Katiba huwezi kuliondoa, kama unataka kuliondoa unapotunga Katiba maana yake ni lazima uvunje muungano.”
Alisema mwaka 1964 mambo yote ya Tanganyika yaliingizwa kwenye Serikali ya Muungano... “Kwa hiyo ni lazima ukafumue Muungano, useme haya ni ya Tanganyika na haya ni ya Muungano,” alisema.
Hamad alisema katika hadidu ya rejea, Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilikatazwa kugusa mambo ya Muungano. “Hivi wabunge 70 wanaokuja kutoka Zanzibar wakazungumzia mambo ya Bara, hivi kuna dhambi gani, sioni kosa kabisa.” Mwenyekiti huyo alisema kamati yake imebaini kwamba Rasimu ya Warioba ina upungufu mwingi kwani hata baadhi ya kero zilizotajwa zilishafanyiwa kazi na Serikali.
Hoja ya ushiriki wa Wazanzibari katika masuala ya Tanzania Bara iliripotiwa kuibuka katika Kamati Namba Moja ambako mmoja wa wajumbe, Ally Keissy alinikuliwa akihoji sababu za wajumbe wa Zanzibar kushiriki mambo ambayo wao siyo sehemu yake.
SOURCE:Mwananchi,Millard Ayo


EmoticonEmoticon